Tuesday, October 28, 2014

Baraza la Biashara Geita lashauriwa kuongeza ubunifu

Na Mwandishi wetu, Geita
Baraza la Biashara la Mkoa wa Geita limetakiwa kuongeza ubunifu ili kuhakikisha mkoa huo unapiga hatua katika nyanja za uwekezaji na biashara ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa mkoa na nchi kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Baraza hilo, Bw. Said Magalula amesema mwishoni mwa wiki akizindua rasmi baraza hilo kuwa wakati umefika kuhakikisha mkoa unakuza uwekezaji na biashara.

“Baraza litumike kukuza biashara katika mkoa wetu ambao una fursa nyingi za uwekezaji,”alisema Bw. Magalula ambaye pia ni mkuu wa mkoa huo.

Mabaraza ya biashara ya mkoa yanaundwa na wadau toka sekta ya umma na binafsi na yanafanya kazi chini ya Baraza la Taifa la Biashara (TNBC).

Alisema kimsingi sekta binafsi ni injini ya maendeleo na inasaidia kukuza uchumi na jambo kubwa ni kwa baraza kufanya kazi kwa bidii na kwa ushirikiano.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, mkoa wa Geita una fursa nyingi na unahitaji wawekezaji katika sekta za madini na viwanda vya kuongeza thamani mazao ya mifugo, Kilimo miongoni mwa nyingine.


Alisema pamoja na kwamba mkoa huo una vikwazo vya biashara, ni wajibu wa baraza hilo kujadili na kutoa mapendekezo ili serikali iweze kutafuta ufumbuzi.

No comments: