Monday, September 30, 2013

Anjouan, Kanda ya Kaskazini wafikia makubaliano ya biashara/uwekezaji



Na Mwandishi wetu, Tanga
Uhusianao kati ya Anjouan, moja ya visiwa vinavyounda nchi ya Comoro na Tanzania unazidi kuimarika baada ya pande hizo kutiliana saini mkataba wa ushirikiano katika maswala ya uwekezaji na biashara kwa faida ya wananchi wao.
Makubaliano hayo yametiwa saini kati ya Anjouan kwa upande mmoja na mikoa minne inayounda kanda ya kaskazini ambayo ni Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara wakati wa kongamano la uwekezaji mwishoni mwa wiki mjini Tanga.  
Gavana wa Kisiwa cha Anjouan, Bw. Anissi Chamsidine, alitia saini kwa niaba ya watu wake wakati mikoa hiyo minne iliwakilishwa na Makatibu Tawala wa mikoa hiyo.
Akiongea muda mfupi kabla hajatia saini yake, Gavana Chamsidine aliwaambia washiriki wa kongamano kuwa kisiwa chake kina soko kubwa la vitu kutoka Tanzania.
“Leteni bidhaa mbalimbali kama mbogamboga, nyama na nyinginezo,” aliwaambia wajumbe hao wa kongamano lililotayarishwa na kituo cha uwekezaji Tanzania (TIC).
Alisema kisiwa chake kina fursa kama za utalii, afya, na elimu ambazo zinahitaji kuendelezwa na kukaribisha watu kuangalia nafasi hizo za kiuchumi kwa faida ya pande zote mbili.
Gavana huyo pamoja na ujumbe wake walihudhuria kongamano hilo kama moja ya ratiba katika ziara yao kuangalia fursa za uwekezaji na biashara hapa nchini.
Wakati wa kongamano hilo, Gavana na ujumbe wake walikutana na wakuu wote wa mikoa, TIC, na maafisa wengine wa serikali kuainisha maeneo ya ushirikiano na namna nzuri ya kushirikiana kwa faida ya pande zote mbili.
Akifunga kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwezeshaji na Uwekezaji, Dkt. Mary Nagu aliwataka wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi wa wilaya kufungua vituo vya kusaidia maswala ya uwekezaji katika maeneo yao ambavyo vitaratibiwa na TIC.
“Vituo hivyo vilenge kupunguza gharama za kufanya biashara hapa nchini,” alisema.
Alifafanua kuwa gharama ya kufanya biashara hapa nchini bado ni kubwa ikilinganishwa na nchini nyingine za Afrika Mashariki na kwamba hilo lazima lifanyiwe kazi ili kuvutia zaidi mitaji na kuleta maendeleo ya haraka.
Alisema ni wakati muafaka sasa kwa kila mkoa kujiwekea malengo yatakayopimwa kila mwaka kuangalia uwekezaji ulioingia katika mkoa husika, changamoto na nini kifanyike kuvutia zaidi uwekezaji.
“Kipimo cha kwanza cha mkakati huo itakua kuangalia idadi ya miradi ya uwekezaji katika mkoa,” alisema.
Alisema katika mkakati huo kila mkoa utatakiwa kuonyesha mipango inayotarajiwa kufanyika katika kipindi fulani.
“TIC itatengeneza ripoti moja kwa ajili ya ufuatiliaji zaidi na utekelezaji kupitia ofisi yangu,” alisema.
Kongamano hilo la siku mbili lililofunguliwa na waziri mkuu Mizengo Pinda lilihudhuriwa na wawekezaji zaidi ya 1,500 toka ndani na nje ya nchi pamoja na maafisa wengine toka sekta binafsi na umma, viongozi wa dini, mabalozi na wadau wengine wa mandeleo.
Mwisho

No comments: