Monday, September 1, 2014

TPSF yasisitiza matumizi ya TEHAMA kuimarisha biashara mipakani

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Bw. Godfrey Simbeye (kulia) akiwa na Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Bw. Haji Janabi wakati wa warsha ya kujadili matokeo ya utafiti kuhusu njia za kuongeza uwazi na kukabiliana na rushwa katika mnyororo wa biashara mipakani mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Bw. Godfrey Simbeye (katikati) akiwa na Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Bw. Haji Janabi (kulia) na Mkurugenzi wa Huduma wa kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mama Nakuala Senzia wakati wa warsha ya kujadili matokeo ya utafiti kuhusu njia za kuongeza uwazi na kukabiliana na rushwa katika mnyororo wa biashara mipakani mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Bw. Godfrey Simbeye (kulia) akiwa na mtaalamu mshauri kutoka kampuni ya Gotham International, Bw. John Kyaruzi wakati wa warsha ya kujadili matokeo ya utafiti kuhusu njia za kuongeza uwazi na kukabiliana na rushwa katika mnyororo wa biashara mipakani mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Tanzania imeshauriwa kujikita zaidi katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuimarisha utendaji wa biashara hasa katika maeneo ya mipakani.

Imesemekana kuwa pamoja na kuwepo kwa mifumo mingi inayoweza kusaidia kuongeza uwazi, kupamabana na rushwa na kuleta ufanisi kwenye mnyororo wa biashara za mipakani, lakini bado mifumo hiyo haitumiki ipasavyo.

Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF) imesema wakati sasa umefika kwa Tanzania kuimarisha matumizi ya mifumo hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Bw. Godfrey Simbeye alisema hayo katika  warsha ya kujadili ripoti ya mshauri mwelekezi kuhusu fursa za kuongeza uwazi na kupambana na rushwa kwenye mnyororo wa biashara za mipakani katika mwendelezo wa tafiti zilizofanywa na sekta yao ili kuimarisha mazingira ya biashara hapa nchini.

“Baadhi ya taasisi hapa nchini zina mifumo hii ukiwemo ule wa Tanzania Customs Integrated System (TANCIS) na ule wa NTBs SMS and Reporting System lakini hakuna utaratibu unaoiwezesha taasisi zingine kuitumia hasa zile za maswala ya biashara,” alisema mwishoni mwa wiki.

Alisema mifumo hiyo inawezesha kuweka sheria na taratibu zote za kibiashara  ili watu waione kwa uwazi zaidi na pia husaidia kufanya mawasiliano yanayolenga kuondoa urasimu na mianya ya rushwa kwa kutoa taarifa kwa vyombo husika.

Pia utafiti huo umeangalia ni jinsi gani wadau mbalimbali wakiwemo wa sekta yao wanatumia mifumo hiyo kwa nia ya kuzidi kuweka mazingira bora ya biashara zikiwemo zile za  mipakani.

Akitoa mfano alisema TCCIA imeweza kuweka mfumo wa kutoa taarifa kwa njia ya SMS popote pale ambapo mtu yupo, hivyo kusaidia kutoa taarifa mbalimbali zikiwemo za vitendo vya rushwa kwa vyombo kama polisi.

“Matokeo ya tafiti hii yatasaidia kutekeleza Mpango wa Matokeo Makubwa sasa (BRN),” alisema.

Alisema TPSF inapongeza juhudi ya serikali ya kuzidi kuondoa vizuizi barabarani kwa kiwango kikubwa na kusema kuwa bado kazi kubwa inatakiwa kufanyika.

Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Bw. Haji Janabi, alisema mifumo hiyo ina fursa kubwa katika kuleta mabadiliko katika utendaji kazi.

“Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi katika uchumi na utoaji ajira na jitihada zinazofanyika ni kuhakikisha mifumo hii inafanya kazi kwa ajili ya kukuza biashara mipakani,” alisema.

Alisema mapendekezo yatakayotolewa kuhusu warsha hiyo yatatumiwa na serikali hasa  wizara hiyo ili kutafuta ufumbuzi katika kuboresha mazingira ya biashara za mipakani.

Naye mtoa mada katika warsha hiyo, Bw. John Kyaruzi toka Kampuni ya Gotham International alisema baadhi ya taasisi zina mifumo hiyo lakini hakuna uratibu wa kuhakikisha inatumiwa na taasisi nyingine.

“Mifumo hii ambayo tayari ipo tukiweza kuwa na uratibu mzuri wa kutumiwa na taasisi mbalimbali tutapiga hatua kubwa,”alisema.

Alisema TCCIA inatumia mfumo wa NTB SMS and Reporting System na bandari inatumia mfumo wa Tanzania Customs Integrated System (TANCIS) ambayo yote kwa pamoja ni ya kisasa na  ina uwezo mkubwa wa kufanya kazi.

Naye msimamizi wa  utafiti huo, Dkt. Donath Olomi alisema licha ya baadhi ya tasisi kuwa na mifumo hiyo ambayo ina uwezo mkubwa wa kutumiwa na taasisi zingine, lakini bado taasisi zingine zinataka kununua mifumo mingine.

“Mifumo hii kuinunua ni gharama sana, mfumo moja unagharimu dola za Kimarekani milioni 50 sawa na bilioni 70 za kitanzania,”alisema na kuongeza kuwa hakuna sababu ya taasisi nyingine kununua kwa vile mifumo iliyopo inaweza kuunganishwa na kutumika kwa shughuli mbalimbali na wengine.

Mwisho 


Watanzania wazingatie matumizi ya maji yanayofaa—Prof. Hulda Swai

Muanzilishi wa kampuni ya Original Water, mzalishaji wa maji ya Eden Mineral Water, Prof. Hulda Swai akionyesha chupa ya maji hayo alipokuwa akiongea na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.  Maji hayo yanatengenezwa na madini muhimu yanayopatikana katika chumvi toka milima ya Himalaya. Kushoto ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Bi. Asenath Mpatwa.
Na Mwandish Wetu, Dar es Salaam
Watanzania wametakiwa kuhakikisha kuwa wanakunywa maji safi, salama na yenye madini yanayotakiwa ili kulinda afya zao.

Ushauri huo umetolewa na Mwanasayansi anayejulikana kimataifa, Prof. Hulda Swai alipokuwa akiongea na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.

Profesa huyo Mtanzania anayefanya kazi katika Chuo Kikuu cha Pretoria nchini Afrika ya Kusini amesema maji yanayofaa kwa matumizi ya binadamu ni yale yenye viwango vinavyotakiwa vya madini.

“Maji si maji tu...maji ni yale yenye madini yanayotakiwa na mwili,” alisema.

Akifafanua zaidi alieleza kuwa yeye kama mwanasayansi amegundua kuwa maji mengi yanayotumika ni maji “mfu” ambayo hayana madini yoyote na kuwa hiyo inasababishwa na mchakato wa kuchuja maji hayo.

Alisema kutokana na uchafuzi wa mazingira uchujwaji wa maji unaofanyika huondoa madini mabaya na yale mazuri na hivyo kufanya maji hayo kutokuwa na faida iliyokusudiwa mwilini.

Ni kutokana na hilo, Prof. Swai anasema amekuja na teknolojia mpya itakayosaidia kuchuja maji na kuongezea madini yanayotokana na chimvi kutoka milima ya Himalaya ambayo ina aina ya madini asilimia 84 kama inavyotakiwa na mwili wa binadamu.

Amesema maji hayo yanayojulikana kama Eden Mineral water yana kiwango sawa maji yaliyotumiwa na mababu na hivyo kuwa na uwezo wa kusaidia mwili kuwa na uwezo wa kupambana na magonjwa na kusafishwa mwili.

“Babu zetu walikunywa maji yenye viwango vizuri sana vya madini na ndio maana hawakupata sana magonjwa kama sasa,” alisema.

Alisema wanatumia teknolojia mpya kabisa kuchuja maji hayo kabla ya kuweka kitaalamu madini yanayotokana na chumvi hiyo ambayo bado haijaharibiwa na uchafuzi wa mazingira.

“Tunatumia teknolojia mpya kabisa ya nano filters 0.1nm...hapa hakuna chembechembe zozote zinazoweza kupenya isipokuwa maji,” alisema Prof. Swai ambaye ni muanzilishi wa kampuni ya Original Water inayotengeneza maji hayo.

Akitaja baadhi ya faida za maji hayo, Prof. Swai alisema maji yanasaidia mwili kufyonza viinilishe kutoka katika chakula tunachokula na kuvisafirisha sehemu mbalimbali za mwili na kuweka kiwango cha alkali mwilini kinachotakiwa.

Alisema pia kutokana na madini yanayopatikana katika chumvi hiyo, maji hayo yana sifa zinazosaidia seli za mwili kuwasiliana kama inavyotakiwa.

“Maji haya pia yanasaidia kupunguza uzito wa mwili, usagaji mzuri wa chakula na kuhifadhi nguvu ya mwili inayotakiwa,” alisema.

Mkurugenzi wa kampuni ya Original Water inayotengeneza maji hayo ya Eden Mineral water, Bi. Asenath Mpatwa alisema maji hayo yamepata muitikio mzuri tangu yaanze kuuzwa na kuwa watu wameanza kufahamu faida zake.

Aliipongeza serikali kwa kuwa na sera inayoruhusu watu binafs kutengeneza maji.

Alisema kampuni yao imesajiliwa na maji hayo yamekaguliwa na kupata idhini ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).

“Sekta ya maji ni moja ya sekta muhimu...maisha ya binadamu yanategemea maji na maji ya kunywa ni muhimu zaidi katika kuendeleza uhai,” alisema Bi. Mpatwa.


Mwisho